Wednesday, March 13, 2013

Mshirika wa Ponda adai polisi walitaka kuwaua msikitini

Mshirika wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, katika kesi ya uvamizi wa eneo la ardhi, Maulid Namdeka amewatupia tuhuma polisi waliowakamata kuwa walitaka kuwaua kwa kuwapiga risasi ndani ya msikiti. Namdeka ambaye ni mshtakiwa wa 38 katika kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu Viktoria Nongwa, wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alitoa tuhuma hizo jana wakati akijitetea akiongozwa na Wakili wake, Juma Nassoro.
Pia, mshtakiwa huyo alikiri kufikia eneo Markaz Chang’ombe kwa ajili ya kushiriki kujenga msikiti, baada ya kutangaziwa na Imamu wa Mskiti wa Yombo kuwa, Waislam wanatakiwa kwenda kushiriki ujenzi wa mskiti huo.
Katika ushidi wake, Namdeka alidai kuwa alifika eneo hilo Oktoba 16, mwaka jana kwa lengo la kushiriki Ibada ya Itikafu na ujenzi wa msikiti huo kesho yake.
Hata hivyo, alidai usiku wakiwa kwenye ibada, walivamiwa na polisi na kwamba kiongozi wa polisi hao aliwaamrisha askari wake wawapige risasi msikitini, lakini askari mmoja alipinga kuwa hawawezi kuwapiga risasi kwa sababu hawana silaha.
Namdeka ambaye alitoa ushahidi huo wa utetezi akiwa shahidi wa 30 upande wa utetezi, alidai baada ya hapo walikamatwa wote na kupelekwa Kituo cha Polisi Mabatini, Kijitonyama.
Tofauti na washtakiwa wengine waliokwishatoa utetezi, wakati akihojiwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka, Namdeka alikiri kutoa maelezo ya onyo yaliyoandikwa na askari mmoja kuhusiana na tuhuma za uvamizi wa eneo hilo.
Habari - James Magai, Mwananchi  
Chanzo - Mwananchi

No comments:

Post a Comment