Friday, January 18, 2013

MIKOPO YAKIMBIZA WALIMU VITUO VYA KAZI MAGU



Walimu wa shule za msingi katika wilaya ya magu mkoani Mwanza,wamekuwa wakitoroka katika vituo vyao vya kazi na kuacha kufundisha kwa kuogopa kukamatwa kutokana na madeni yanayotokana na kukopa kutoka kwa watu binafsi.
Hayo yameelezwa juzi (16/01/2013)na Ofisa Elimu wa shule za msingi wilayani Magu, Yesse Kanyuma kwenye kikao cha kazi cha viongozi wa elimu wa wilaya,waratibu elimu kata, walimu wakuu na walimu wakuu wasaidizi kilichofanyika ukumbi wa CCM Mjini Magu.

Kanyuma alisema kuwa baadhi ya walimu wilayani hapa, wameshindwa kufundisha na wamekuwa wakitoroka kwenye vituo vyao vya kazi kutokana na kudaiwa na wakopeshaji hao ambao wamekuwa wakichukua kadi zao za ATM za benki kwa makubaliano ya kulipa mkopo  kwa riba ya asilimia 50 mpaka 100, kiwango ambacho ni kikubwa mno.

Alisema kuwa, kutokana na hali hiyo kiwango cha taaluma katika shule zao kimeshuka sana, na kwamba baadhi ya walimu anaodaiwa na watu hao wameshitakiwa mahakamani kwani wameandikiwa mikataba na wakopeshaji hao ambao sio rasmi kisheria.

Aidha, wakati kikao hicho kikiendelea, walimu wawili waliletewa barua za wito mahakani kutokana na kushindwa kulipa kwa wakati mikopo waliyokopeshwa na wakopeshaji hao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa wilaya ya Magu, Bi Naomi Nnko amekemea tabia ya utoro wa walimu na wanafunzi katika shule za wilaya hiyo.


No comments:

Post a Comment