Wednesday, March 20, 2013

Wakulima A. Mashariki wahimizwa kuungana

RAIS wa Shirikisho la Wakulima wa Afrika Mashariki, Philip Kiriro, amewataka wakulima wadogo kuungana katika kupigania maslahi yao, ili kujikomboa kutoka kwenye ukulima mdogo hadi mkubwa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kiriro alisema iwapo wakulima hao hawataungana mafanikio yao hayatakuwa mbali.
Alisema shirikisho hilo lenye makao makuu nchini Kenya, limekusudia kuwaunganisha wakulima kwa lengo la kuwa na sauti moja katika maamuzi yao ambapo litafanya kazi na serikari za nchi hizo.
“Tumekuja hapa nchini kukutana na Shirikisho la Vyama Ushirika, pia kutembelea ofisi za serikali na kuifahamisha serikali juu ya shirikisho hilo litakavyofanya kazi na wakulima wadogo katika nchi za Afrika Mashariki,” alisema Kiriro.
Aidha alisema kati ya nchi zilizopo kwenye jumuia hiyo, Tanzania ina fursa ya kufanya vizuri katika kilimo kutokana na kuwa na maeneo makubwa kwa shughuli za kilimo.
Naye Katibu Mtendaji wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika (TCC), Willings Mbogo, alisema watahakikisha kupitia shirikisho hilo wanakuza uwezo wa wakulima wadogo na wajasiriamali, ili waweze kukuza uchumi kutoka katika hali ya sasa na kuufanya uwe bora zaidi.

No comments:

Post a Comment