Wednesday, March 20, 2013

TPSF yapongezwa kuimarisha sekta binafsi nchini

TAASISI ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) imepongezwa kwa jitihada inazochukua hivi sasa kuhakikisha kuwa sekta hiyo inakuwa imara, sauti moja na hivyo kuchangia zaidi katika ujenzi wa uchumi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jijini Mwanza hivi karibuni, Jovita Bubere na Moses Nyaronga, walisema TPSF imesaidia kwa kiasi kikubwa kukuza biashara zao na kuongeza mitaji.
“Tunaomba taasisi hii iendelee na jitihada zake za kuwasaidia wanachama wake mikoani, ili kuendelea kutujenga katika kukuza biashara hasa kwa mikutano kama hii ya kikanda,” alisema Bubere wakati wa mkutano ulioshirikisha wanachama wa TPSF Kanda ya Ziwa.
Bubere ambaye ni Mwenyekiti wa Asasi ya kinamama Wajasiriamali Tanzania, alisema: “Tunahitaji msaada mkubwa ili kuweza kufikia malengo yetu.”
Akizungumzia soko la Afrika Mashariki, mwenyekiti huyo alisema wamejipanga vizuri na tayari wameshaanza kutoa mafunzo kwa baadhi ya kinamama kuhusiana na mbinu za kutumia ushindani unaokuja wa kibiashara.
Kwa upande wake, Nyaronga ambaye ni Mwenyekiti wa Shirika la Lemon Development Foundation lililoko katika wilaya ya Rolya, mkoani Mara, alisema huu ndio wakati wa kuiunga mkono TPSF, ili iweze kufanya kazi kwa uhakika zaidi ya ilivyo sasa.
Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Geofrey Simbeye, alisema taasisi hiyo ina lengo la kuweka mazingira bora na wezeshi kwa wanachama wake katika kuongeza kasi ya uanzishwaji wa makampuni na viwanda kwa ajili ya kuongeza ajira na kuinua uchumi wa nchi.

No comments:

Post a Comment